Thursday, March 3, 2016

Mdee, Waitara wapanda kizimbani



 WABUNGE wawili, Halima Mdee (Kawe) na Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara na wanachama wengine wa Chadema wamepandishwa kizimbani wakikabiliwa na mashitaka ya kumjeruhi Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam, Theresa Mmbando.

Wengine waliopandishwa ni Diwani wa kata ya Saranga, Kinondoni, Ephraimu Kinyafu pamoja na mwanachama wa Chadema, Rafii Juma.

Watu hao walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi. Mwenyekiti wa wabunge na madiwani wa Ukawa, Manas Mjema ambaye pia anakabiliwa na mashitaka hayo hakufika mahakamani hapo.

Washitakiwa walifikishwa mahakamani jana mchana wakiwa chini ya ulinzi wa Jeshi la Polisi, wakitoka Kituo Kikuu Kanda ya Dar es Salaam.

Akiwasomea mashitaka, Wakili wa Serikali, Mwaanamina Kombakono alidai kuwa Februari 27, mwaka huu katika Viwanja vya Karimjee Dar es Salaam, kwa pamoja washtakiwa walimjeruhi Mmbando na kumsababishia majeraha mbalimbali kwenye mwili wake.

Washitakiwa walikana mashitaka, na upande wa Jamhuri ulidai upelelezi wa shauri hilo haujakamilika, hivyo wanaomba tarehe nyingine ya kutajwa. Pia waliiomba mahakama itoe hati ya mwito wa kuitwa Mjema kutokana na kitendo chake cha kutofika mahakamani.

Chanzo Habari Leo.

No comments:

Post a Comment